Mbunge wa 
viti maalumu (CCM), Jackline Ngonyani jana alizua kizaazaa bungeni baada
 ya kuwaambia wabunge wa upinzani wamekosa dira kiasi cha kula 
rambirambi zilizotolewa kwenye msiba wa Philemon Ndesamburo.
Alitoa kauli
 hiyo alipokuwa akichangia mjadala wa bajeti ya mwaka 2017/18. Baada ya 
kuzungumzia hoja zake, Ngonyani alielezea kilichotokea kwenye salamu za 
pole zilizotolewa wakati wa msiba wa muasisi huyo wa Chadema aliyewahi 
pia kuwa mbunge wa Moshi Mjini kwa vipindi vitatu mfululizo.
Mbunge huyo 
alianza kwa kumpongeza Rais John Magufuli kwa utekelezaji wa ilani ya 
CCM na utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo inawagusa wananchi, 
akidai utekelezaji huo unawanyima hoja wapinzani.
Aliyafananisha
 maneno ya wapinzani na miti kuteleza siku ya kifo cha nyani, akisema 
licha ya kueleza kwamba Rais anatumia sera zao, wapinzani hao wamesahau 
changamoto zinazowakabili wananchi kwenye majimbo yao.
Mbunge huyo alimshambulia mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche na wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari.
Alimshangaa 
Heche kwa kuomba muongozo kutokana na wananchi wa jimbo lake kuvamia 
mgodi wa North Mara ulio chini ya kampuni ya Acacia baada ya kukabiliana
 na askari polisi.
Mwenyekiti 
wa kikao hicho, Mussa Azzan Zungu alimtaka kuwasiliana na Waziri wa 
Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba kupata ufafanuzi wa suala hilo kutoka 
serikalini.
“Huyu Heche 
aliongea humu ndani kuhusu wananchi wake kulinda mgodi, leo anajikosha 
kwa kuomba muongozo. Rais hakusema watu wakavamie migodi, hao wakamatwe 
kama wahalifu wengine. Huyu naye akamatwe na kuunganishwa pamoja na 
wavamizi hao,” alisema.
Baada ya 
kauli hiyo, Heche alisimama na kumpa taarifa mbunge huyo kwa kueleza 
kwamba jina lake linatumika vibaya. Alikumbusha kwamba wananchi wake 
walifuatilia uwasilishaji wa ripoti ya kamati na kufahamu kwamba kampuni
 hiyo ni feki.
“Nilisema sisi tumeumizwa, sasa kama unafikiri naogopa kuunganishwa hebu njoo unikamate wewe,” alisema.
Baada ya taarifa hiyo, Jackline alimwambia Heche: “Usinipotezee muda, nina mambo mengi ya kuzungumza.”
Baada ya 
kuachana na Heche, mbunge huyo alimvaa Nasari kwa kueleza kwamba 
alitumia dakika 10 alizopewa kulalamika juu ya uharibifu uliofanywa 
kwenye shamba la maua la mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.
“Hizi ni 
akili au matope? Wananchi wake hawana changamoto? Ni mambo ya aibu 
sana,” alisema mbunge huyo akikaribia kuhitimisha mchango wake kwenye 
mjadala huo.
Kabla 
hajakaa, sauti ilisikika ikimkumbusha suala la kuliwa kwa fedha za msiba
 huo, kengele ya kuisha kwa muda wake ikiwa imeshagongwa, alitupa 
kijembe wa upinzani.
“Nakushukuru sana mwenyekiti, naunga mkono hoja na (wapinzani) waache kula rambirambi za msiba wa Ndesamburo,” alisema Ngonyani.
Kauli hiyo iliwafanya wabunge wa upinzani wacharuke na kumtaka afute maneno hayo.
Alikuwa ni 
mbunge wa viti maalumu (Chadema), Cecilia Pareso aliyemng’ang’ania baada
 ya kutoa taarifa kwamba kilichozungumzwa na Jackline si sahihi na 
kumtaka kufuta maneno hayo au kuthibitisha tuhuma hizo.
Mbunge huyo alikubali kuyaondoa maneno yake kwenye kumbukumbu kutokana na kukosa ushahidi wa alichokisema.
“Mwenyekiti,
 kwa sababu ni suala la msiba, nayaondoa maneno hayo,” alisema na 
kuhitimisha suala hilo lililowagusa wabunge wengi wa upinzani 
waliokuwapo kwenye kikao cha jana asubuhi.

No comments:
Post a Comment